
WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Makazi,Profesa Anna Tibaijuka amesema kuwa hawezi kujiuzulu katika nafasi ya uwaziri kutokana fedha ya Tegeta ESCROW.
Akizungumza na Waandishi na Habari mapema leo jijini Dar es Salaam katika ukumbi wa Hoteli ya Hayyat Regency, Profesa Tibaijuka alisema kuwa udalali wake wa fedha hiyo ni kwa ajili ya wanafunzi katika shule za Taasisi ya Barbo Johansson Girls Education Trust, na kwamba fedha aliyoipata ni Bilioni Tshs. 1.66 ambazo zilitoka katika kampuni ya James Rugemalira kama msaada kwa shule hiyo.
Alisema kuwa fedha hiyo kuingia katika akauti yake binafsi ilitokana na masharti ya mtoa msaada ndugu James Rugemalira ambaye alitaka fedha hiyo iingie katika akauti ya Benki ya Mkombozi.
"Nikijiuzulu hata Rais Jakaya Kikwete atanishangaa kwani fedha nilizopata ni za shule na kwa ajili kukomboa elimu nchini hasa kwa watoto wa kike kutokana na wazazi wengi kutoweza kumudu gharama za shule’’alisema.
Alisema kuwa udalali wake ni kutafuta fedha kwa ajili ya elimu nchini ambapo, alidai hata Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP Dkt Reginald Mengi alitoa sh.milioni 248 kwa ajili ya msaada wa shule hiyo.
Profesa Tibaijuka alisema kuwa wananchi watambue kuwa yeye ni mstaafu wa Umoja wa Mataifa hivyo hawezi kufanya hivyo na kama angetaka fedha hiyo angeweza kufuata hata katika shule na kuchukua.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Makazi,Profesa Anna Tibaijuka akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kwenye hoteli ya Hyatt Regency,Jijini Dar es salaam leo.

NA CHALILA KIBUDA WA MICHUZI MEDIA.